0
RIWAYA: ROHO MKONONI
MTUNZI:George Iron Mosenya

                                   
SEHEMU YA NNE


Wakabaki kuwatazama jinsi walivyolia huku wakiwa wamekumbatiana. Dada mkuu Betty, alimwongoza Joyce hadi chini ya mti. Hatimaye wakasimuliana yote yaliyotokea, Betty hakuwa na jipya sana maana kifo cha mama yake kwa ajali ya meli kilikuwa kinafahamika.
”Betty inaniuma sana sikuweza kumuona mama kwa mara ya mwisho…. Ziwa Viktoria liliamua kunipa uchungu wa milele…lilimmeza mama yangu, na halikutaka kumtapika tena.” Aliongea huku akibubujikwa na machozi.
Ni heri yeye alijua ni jinsi gani mama yake alipoteza uhai.
Simulizi ya Joyce Kisanga ilianzia siku ambayo anatarajia kusafiri kwenda Mwanza.
Akafumba macho alipomueleza Betty alichokikuta sebuleni. Mwili wa mama yake mdogo ukiwa umetapakaa chini huku damu zikimvuja. Baada ya hapo akapoteza fahamu na kuzinduka tena akiwa hospitali ya Murutunguru. Huko alipewa huduma zilezile za kawaida. Kisha akarejeshwa nyumbani.
“Betty nilikuta umati wa watu pale nyumbani nikajiuliza kulikoni, nini kimetokea. Wazo langu la kwanza na kuu likawa huenda ma’mdogo atakuwa amekufa. Betty ni bora uwaze jambo fulani maishani na kisha lisiwepo kuliko kutoliwaza halafu unalikuta…Joy uchungu huu hautaisha kamwe rafiki yangu. Eti nakuta taarifa kuwa mama yangu………” Joy akaanza kulia Betty akambembeleza, akatulia na kuendelea, “mama alikuwa ameuwawa Betty….na bora basi angekuwa mama mwenyewe..na ma’mdogo ambaye nd’o ilikuwa mara ya kwanza kuja kijijini na alikuja kwa ajili yangu tu jamanii…ma’mdogo naye alifia sebuleni kwetu alifia eneo lile ambalo nilikuwa natandika mkeka usiku nalala.” Akakoma akajifuta machozi na kupenga kamasi nyepesi.
“Sasa baba yupo wapi, hakika hilo ni pigo mpenzi” Betty alisema bila kumtazama Joy machoni.
“Halafu ikamalizikia nyundo ya mwisho Betty wangu…na mzee Kisanga huyo unayeulizia yuko wapi alikutwa kichakani amejinyonga kwa kutumia kanga ya mama yangu….” Hapa sasa kilio kikawa kikubwa sana. Betty akafanya kazi ya ziada kumtuliza rafiki yake.


Mwalimu mkuu akafika eneo lile lakini kwa uchungu wa waziwazi aliouona hakutaka kuuliza chochote naye akawaacha kwa muda.
Joyce akajielezea juu ya mume wa mama yake mdogo alivyomchukua kwa ajili ya kumsomesha lakini chuki kutoka kwa ndugu walioweka imani za kishirikina mbele kuwa mkewe aliuliwa maksudi kwa ajili ya kafara zikasababisha amani kutoweka na baada ya mwaka miaka miwili akaamua kumleta Njombe kwa aliyetakiwa kumuita mjomba.
Hapa akaelezea juu ya shule ya msingi Kifanya na balaa alilomfanyia dada mkuu.
“He! Joy kumbe ni wewe uliyemuadabisha” hapa sasa Betty akatabasamu.
“Aliniletea ujinga wakati nina uchungu. Hakika nilimwadabisha sikufichi…nilimsulubu, na wangenipa walau dakika kumi nyingine za nyongeza angewafuata akina mzee Kisanga huko mbinguni mi sijui.” Alijibu kwa jazba kuu.
“Sasa mbona walisema ni Keto nd’o kafanya hivyo.”
“Yeah kwa sasa naitwa jina hilo na hata baada ya kufukuzwa nimeondoka na jina hilo hilo kuja hapa. Hilo jina nimelikuta pale shuleni kuna mwanafunzi aliacha shule anaitwa hivyo. Joyce Keto.” Alimaliza maelezo.
Sasa kidogo walikuwa wanatabasamu. Marafiki wa kufa na kuzikana. Kutoka Ukala Ukerewe sasa wanakutana, Makambako Iringa (sasa Njombe).
“Nilidhani shule nimerudia mimi peke yangu kumbe na wewe mwenzangu umerudia, sa’hivi si tulitakiwa kuwa Kidato cha kwanza sijui cha pili” alisema Joyce, kwa pamoja wakacheka.
Dada mkuu Betty akamuongoza rafiki yake wa dhati hadi mgahawani. Wakaagiza chai.
Wakati wanakunywa chai, Betty alitumia fursa hiyo kumweleza maisha yake ya huko Makambako. Alikuwa akiishi kwa mjomba wake pia ambaye alimchukua baada ya mama yake kukumbwa na umauti. Alimchukua akiwa darasa la sita lakini walipofika Makambako alilazimika kurudia darasa la nne ili aweze kusajiliwa kwa jina lake la kuzaliwa.
Alijieleza mengi sana juu ya maisha ya kawaida anayoishi na mjomba wake. Lakini walau alikuwa ana furaha na ukiwa ulikuwa umepungua.
“Heri yako Betty, yaani mimi huku ni ilimradi, hebu nitazame…” alikata kauli kisha akamwonyesha Betty mwili wake jinsi ulivyopauka. Halafu akaendelea “maisha ni magumu pale yaani magumu sana, bora nilipokuwa Kifanya huko maisha yalikuwa yana unafuu. Sema namshukuru Mungu bora uzima.”
Betty akaguna huku akibetua mabega yake. Akaimalizia chai yake wakasimama na kuondoka baada ya kulipia huduma.,
Baada ya muda mrefu ule wa utengano, umoja ukaunganika huku wote wakiwa YATIMA!!
Kubwa zaidi walikuwa wanafunzi wa shule moja. Shule ya msingi Namvura. Maisha yakaendelea, wawili hawa wakiwa darasa moja, darasa la sita katika shule hiyo.
Joyce akiwa na miaka kumi na saba huku Betty akiwa anamzidi kwa miezi mitatu tu….
Licha ya umri wao miili yao iliwabeba, si kwamba ilikuwa miili midogo sana la! Palikuwa na wanafunzi wakubwa zaidi yao.
Miaka ile hapakuwa na utaratibu wa kumpeleka mtoto wa miaka minne darasa la kwanza kisa tu ana uwezo mkubwa wa kuelewa.
Umri mkubwa ulipewa kipaumbele kwanza.
Sina imani kama dhana hii ilimaanisha ukubwa wa mwili na umri nd’o wepesi wa kuelewa!!!
Lakini ilikuwa hivyo kwa miaka ile.
Miaka ambayo shule za awali ziliheshimika sana. Ilikuwa nadra kwa mtoto kutokea nyumbani moja kwa moja na kujiunga na darasa la kwanza bila kupitia shule ya awali.






****
MAKAMBAKO IRINGA (Sasa Njombe), 2000.


Redio iliyosikika kwa kukwaruza kiasi fulani kutokana na mawimbi kutokamatika barabara katika kijiji chao ilitangaza jambo lililomshtua mzee Kamese. Kama kawaida yake hakuwa mtu wa kukurupuka, akatulia aweze kusikiliza vyema taarifa ile kiundani. Hakika ilikuwa kama alivyoisikia awali.

Hapo sasa aliweza kunyanyuka katika kiti chake cha kamba, akajinyoosha kidogo huku akiiweka vyema suruali yake kiunoni.
“Mke wangu weeee!! ….mama watoooo” sauti yake ya kukoroma ambayo ilifanania na mtu ambaye amebanwa na kikohozi sasa anataka kukohoa lakini kabla ya kukohoa anajikuta kuna jambo la msingi la kuongea kabla hajakohoa.
Lakini kwa huyu haikuwa hivyo, umri wake ulikuwa mkubwa sana. Na sauti nayo ikawa imefikia kikomo. Kwa jinsi alivyoita ungeweza kutarajia mkewe huyo anayemuita angeweza kuwa kikongwe asiyeweza kusimama wima tena na uso wake hautabasamu vizuri na meno yaliyotoka kichwani ni mengi zaidi ya yale yaliyosalia.
Ilianza kusikika sauti ikiitika. “Bee mume wangu!” ilikuwa sauti nyororo na kama ingekuwa inatoka kwa kikongwe basi angekuwa kikongwe wa maajabu. Mzee Kamese akatabasamu mapengo yakaonekana, hiyo ni baada ya kusikia sauti ile.
Macho yake yakawa makini, mlango ukafunguliwa, ukatangulia uso kuchungulia. Wakakutana ana kwa na mapengo yakawa yanatazamana na mwanya maridadi.
“Mke wangu huyooo….mwanyaaa.” mzee Kamese akasema kwa sauti yake ileile ya kukwaruza. Mwanamke aliyekuwa mlango akajiziba uso kisha akaanza kulalamika, “Babu mi s’takiii, unanicheka na mwanya wangu”
Mzee Kamese akacheka kwa sauti ya juu kidogo kisha akaketi tena na yule binti akaketi karibu yake.

“Hapo unataka ugolo wako au mapombe yako, mi n’takuwa sikubusu tena shauri zako.” Kwa sauti inayoshawishi kuendelea kusikiliza hata kama anazungumza ujinga binti alilalamika kiutani.
“Mh!! Hayo nilishaacha mke wangu, leo nina habari njema sana.”
“Mwee! We nawe babu cha uongo ka’ nini habari gani?” aliuliza kwa kiherehere.
“Nipe mji kwanza….” Babu akazuga, binti akajifanya kununa. Babu akamwita kisha akamnong’oneza.
Binti akaruka juu kwa shangwe.
“Babu usije kuwa unanitania babu…” alilalamika.
“Betty mjukuu wangu, mimi nakuombea Baraka tele ufanikiwe kujiunga na kidato cha kwanza, naombea matokeo yako wewe na yule rafiki yako nani yulee…..”
“Joyce!” Betty akamalizia, “Ehee huyohuyo, kati ya marafiki zako yule nd’o rafiki sasa mjukuu wangu achana na wale wengine sijui wana tabia za wapi wale….”
“Babu kwa hiyo yapo wapi hayo matokeo.”
“Wilayani pale kesho alfajiri kimbia mapema ukajionee kama umechaguliwa. Nakuombea heri mwanangu….haya nenda kaoshe vyombo maana najua nimekukurupusha huko…mtazame na masabuni yake mikononi huyooo” Akamalizia babu, mjukuu akatimua mbio huku akilalamika.
Hakika ilifurahisha kuwatazama!!

Saa kumi na moja alfajiri Betty akiwa ameuhifadhi mwili wake katika jaketi kubwa na zito kabisa, alikuwa akitembea upesi upesi, hakuwa akielekea wilayani la! Alikuwa anaelekea mahali pengine kabisa.
Kiza bado kilikuwa kimeitawala anga lakini hilo halikumpa hofu. Alipoifikia nyumba aligonga mlango kwa sauti ya chini kidogo. Akamsikia mtu akijigeuza pale kitandani.
“Nani?” sauti ya kukoroma iliuliza.
Alikuwa ni Joyce
“We Joyce wewe amka…amka Joy!” sauti ya Betty ilisihi. Mchakato ukasikika tena, kisha hatua zikafuata, mlango ukafunguliwa. Joyce alikuwa katika dimbwi la usingizi bado, usiku uliopita alichelewa sana kulala.
“Joyce matokeo yametoka mwenzangu.” Betty alimweleza hatimaye, taarifa hii ikauondosha usingizi wake.
Baada ya dakika kumi wawili hawa walikuwa barabarani wakitimka mchakamchaka kuelekea wilayani. Licha ya unene aliokuwa ameupata, bado Betty alikuwa na spidi katika kukimbia, Joyce alikuwa akimshangaa ni kwa jinsi gani Betty aliweza kukimbia kiasi kile wakati alikuwa amenenepa tofauti na alivyokuwa wakati wapo Ukala.

Hatimaye wakafika wilayani, matokeo yakiwa na takribani nusu saa tangu yabandikwe. Macho yakisaidiwa na vidole yakaanza kutafuta majina yaliyokuwa ukutani.
Wa kwanza kushangilia alikuwa Betty, na dakika chache baadaye furaha ikawa kubwa zaidi. Joyce Keto naye alikuwa amechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza. Furaha ikazidi kipimo, wote walikuwa wamechaguliwa kujiunga na shule moja ya upili. Kwa maana hiyo wataendekea tena kuwa pamoja.
Ilikuwa siku ya kipekee, walijipongeza kwa kila neno waliloweza kusema kwa vinywa vyao. Siku hii ikaisha huku kila mmoja akiiona kuwa ya kipekee sana. Huenda siku ya kipekee kupita zote.

Haikuwa kama wanavyodhani kuwa furaha yao itadumu kwa muda mrefu huku wakitimiza ndoto zao bila vikwazo vyovyote. Asubuhi iliyofuata Betty mwenye furaha akafunga safari tena kwenda nyumbani kwao Joyce. Nia ikiwa kumkaribisha nyumbani kwao ambapo alikuwa amechinjiwa kuku kama namna ya kumpongeza.
Aliyefanya yote haya alikuwa mzee Kamese yule babu yake Betty aliyekuwa wa kwanza kusikia katika redio kuwa matokeo yametoka na sasa mjukuu wake alikuwa ameyaona tayari na alikuwa amechaguliwa kuendelea mbele. Kuku mkubwa wa kienyeji akaandaliwa, ubwabwa ukatiwa nakshi kadha wa kadha ili uwe na utofauti.
Betty akafanywa mtu maalum siku hiyo, akaambiwa awaalike marafiki zake wasiozidi wanne. Sasa anaanza na Joyce yule rafiki yake wa dhati.

Haikuwa mpaka afike nyumbani kwa akina Joyce la! Alikutana naye njiani, Betty alikuwa wa kwanza kumuona akajificha mahali ili aweze kumshtukiza. Lakini kabla hajafanya hivyo alisikia kilio. Joyce alikuwa analia.
Betty akaghairisha mpango wake, akajongea taratibu. Macho yake yakagongana na yale ya Joyce. Wakatazamana kwa muda kisha Joyce akaangua kilio kikubwa baada ya Betty kumkumbatia. Kilikuwa kilio kikubwa haswaa.
Betty akatumia busara na kumwongoza hadi chini ya mti. Joyce akasina kwa muda kisha akamsimulia Betty chanzo cha kilio chake.
“Eti hawana pesa ya kunilipia ada, na kukaa nyumbani haiwezekani…eti Betty wanataka niolewe….” Hapa akashindwa kuendelea zaidi akaangua kilio upya. Betty akajikaza asiweze kutokwa machozi kwani angekosekana wa kumbembeleza mwenzake.
Ilikuwa taarifa ya kushtua sana ambayo Betty hakuitegemea kabisa. Lakini Joy alimuhakikishia kuwa hiyo aliyoambiwa ni amri na wala si ombi.

“Eti cha muhimu nimejua kusoma na kuandika hivyo niolewe eti huyo mume wangu ataniendeleza kielimu hapo baadaye…sasa bora hata huyo mume angekuwa mume kweli, yaani anao wake wawili na watoto ni mkubwa umri wa marehemu baba yangu. Betty mi sitakiiii, sitaki kuolewa Betty!!!” aligalagala chini Joyce huku akilia kwa uchungu. Betty ambaye naye alikuwa anatiririkwa machozi kimya kimya alifanya bidii ya kumtuliza. Lakini alikosa neno lolote la kumtuliza na kumpa matumaini. Maana yeye binafsi pia alikuwa ni yatima. Betty alikuwa akizilaani ndoa za mitaara, sasa rafiki yake anataka kuolewa huko!!! Atafanya nini sasa? Hili likawa swali gumu katika mtihani wa muhimu.
Ghafla katika kujigalagaza huku na kule kitu kikachomoka kutoka katika nguo za Joyce, Betty akakikwapua mara moja na kukitazama vyema. Joyce akakoma kulia naye akawa anamtazama Betty.
“Joy mpenzi……hii sio sumu ya panya hii? Ni yenyewe Joy unaipeleka wapi hii….” Betty akiwa ameduwqa alimuuliza Joy.
“Bora nife Betty. Bora nife tu, kuishi na yule mwanaume kama mume wangu ni nusu ya kifo tu….alikuja nyumbani akiwa amelewa mapombe ya kienyeji, mbele ya watu wazima akaanza kunishika shika huku….sio kifo kile.” Alilalamika huku machozi yakimtiririka.

“Joy….kama kweli una mpango wa kujiua na hukunishirikisha, kamwe nisingekusamehe katika maisha yangu, nisingekusamehe kwa ubinafsi huo uliotaka kuufanya. Kwa nini hukunishirikisha, kumbe mimi si rafiki yako Joy…kumbe sina maana kwako mimi si ndiyo…Joy unataka kujiua unikimbie mimi si nd’o hivyo….nasema na wewe Joy. Yaani kukuthamini kote huku, kila mmoja anatambua mimi na wewe ni kama mapacha. Leo hii unataka kujiua …haya jiue Joy nenda ukajiue na dakika moja baada ya kifo chako tutakutana mbinguni ili nikwambie kuwa sitakusamehe kamwe kwa jambo hilo. Kufa name nakuja huko.” Betty aling’aka kisha akaanza kupiga hatua aweze kutoweka. Ikawa zamu ya Joy kubembeleza huku akiomba msamaha.
Hakika nguvu ya upendo inashinda nguvu zote, wakakumbatiana tena na kusameheana.
*****

SHEREHE hiyo ndogo ilipooza sana, Betty alijilazimisha kufurahi lakini kila alipogundua kluwa Joy hana furaha na yeye alifadhaika. Chakula kikalika na sherehe ikaishia hapo. Joyce akarejea nyumbani kwao, Betty akabaki nyumbani.


Usiku huu ulikuwa wa aina yake, Betty ambaye sasa alikuwa binti mkubwa tu. Miaka kumi na saba si haba alikuwa akijaribu kuwaza kiutu uzima ni kipi afanye aweze kumsaidia rafiki yake walau kupata tumaini jipya.
Aliamini kuwa familia aliyokuwa anaishi kamwe isingeweza kumsaidia kwa hili. Akamfikiria babu yake na kuwaza kuwa laiti kama angelikuwa na pesa angeweza kumsaidia, lakini hakuwa na pesa naye alikuwa anatunzwa tu pale.
Akafikiria ni wapi pengine anaweza kupata pesa, hakupata jibu. Na hapakuwa na njia yoyote ya kufanya haya bila pesa. Kwani ukiweka ada pembeni, yalihitajika madaftari, vitabu na sare za shule. Mara akamfikiria Dulla, hapa hakuumiza kichwa chake, kijana yule asingeweza kumsaidia kwa lolote.
Hatimaye akapitiwa na usingizi mzito bila kuwa na jibu sahihi. Cha ajabu asubuhi aliamka akiamini kuwa usiku alipata jibu. Na hili jibu alitakiwa kulifanyia kazi ili aone kama inawezekana kumpa furaha Joy.
Lilikuwa jibu la maajabu sana, yeye binafsi alishangaa kwa nini lile liwe jibu!! Lakini likabakia kuwa jibu sahihi.
****

****FURAHA imetoweka ndani ya muda mfupi JOYCE anasisitizwa juu ya kuolewa……hakuna wa kumsomesha…..anafikia uamuzi wa kujiua, na anaapa kuwa ni heri kufa kamili kuliko kufa nusu katika ndoa ile ya mitaara…..NINI KITAENDELEA. JE ATAOLEWA???


***KUNA jibu Betty amelipata ndotoni, anaamua kulifanyia kazi kwa ajili ya kumkomboa rafiki….Je jibu la ndotoni litafanya kazi mchana kweupe???

Post a Comment Blogger

 
Top