0
Huku zikiwa zimebaki siku 45 kuanzia leo kabla ya kufikiwa siku ya kupiga kura Oktoba 25 mwaka huu, imedhihirika kuwa wagombea wote wa nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwamo Dk. John Magufuli wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Edward Lowassa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), watalazimika kufanya kazi ya ziada kushawishi wapigakura wa mikoa tisa ili kujihakikishia ushindi.

Uchunguzi uliofanywa na Nipashe umebaini kuwa mikoa hiyo tisa, ikiwamo yenye majiji makubwa ya Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya, ndiyo yenye watu wengi zaidi waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura kwa kutumia mfumo wa Kielektroniki (BVR).

Takwimu zilizokusanywa na Nipashe kwa siku kadhaa kutoka katika ofisi za waratibu wa uchaguzi wa mikoa mbalimbali nchini zinaonyesha kuwa kwa ujumla, mikoa hiyo tisa ina jeuri ya kutoa rais ajaye kwani ina mtaji wa kura zinazozidi asilimia 50.

Taarifa za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) zinaonyesha kuwa hadi kufikia Julai 30, 2015 na hata baada ya kuongezwa siku nyingine nne katika wiki ya kwanza ya Agosti, 2015 ili kukamilisha kazi ya uandikishaji kwa kutumia BVR, idadi ya Watanzania waliojiandikisha ilifikia 23,782,558, sawa na asilimia 99.5 ya matarajio. Kati ya hao, Nipashe imebaini kuwa watu 12,119,263 wanatoka katika mikoa tisa inayoongozwa na Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya; na ambayo kimahesabu ni sawa na asilimia 50.96 ya watu wote waliojiandikisha.

Kwa mujibu wa takwimu hizo ambazo sasa zinasubiri matokeo ya kazi ya uhakiki wa NEC iliyohitimishwa juzi ili kutambuliwa kama idadi rasmi ya wapigakura, rais ajaye anaweza kupatikana kirahisi ikiwa atafanikiwa kushawishi wananchi wa mikoa hiyo kujitokeza wote siku ya kupiga kura na kumchagua yeye kwa asilimia 100. Hii maana yake ni kwamba mhusika atavuna kura zinazovuka asilimia 50 na hivyo kumsafishia njia ya kwenda Ikulu kumrithi Rais Jakaya Kikwete anayemaliza muda wake kwani kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi, mshindi huwa ni yule anayepata kura nyingi kulinganisha na washindani.

Mbali na Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya, mikoa mingine kati ya tisa iliyo na mtaji mkubwa wa kura zinazotosha kutoa mshindi wa urais Oktoba 25 ni Tanga, Arusha, Morogoro, Tabora, Dodoma na Kagera.

Dk. Magufuli wa CCM na Lowassa wa Chadema anayewakilisha pia muungano wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vya NCCR-Mageuzi, NLD na Chama cha Wananchi (CUF), wanachuana pia na Fahmy Dovutwa wa UPDP, Hashim Rungwe wa Chama cha Umma (Chauma), Maximillian Lymo wa TLP, Anna Mghwira wa ACT-Wazalendo, Chief Lutasola Yemba wa ADC na Janken Kasambala wa NRA.

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977, Ibara ya 41 (6), inaeleza kuwa mgombea yeyote wa nafasi ya urais atakayepata kura nyingi dhidi ya wagombea wengine ndiye atakayetangazwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, Sheria ya Taifa ya Uchaguzi ya Mwaka 1985 (Sura ya 343), vifungu vya 35E na 35F inatoa mamlaka kwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kumtangaza mgombea aliyepata kura nyingi kuwa mshindi wa nafasi ya urais.

Kwa sababu hiyo, mgombea yeyote atakayefanikiwa kupata asilimia 100 ya kura katika mikoa hiyo tisa atajihakikishia kuwa rais ajaye kwa ushindi wa zaidi ya asilimia 50, hata kama atapata kura za idadi ndogo katika maeneo mengine ya nchi.

WALIOJIANDIKISHA MIKOA TISA
Takwimu hizo za waliojiandikisha BVR zinaonyesha , Dar es Salaam ndiyo kinara kwani imeandikisha watu 2,845,256, sawa na asilimia 11.97 ya watu wote waliojiandikisha; Mwanza inashika nafasi ya pili baada ya kuandikisha watu 1,442,391 ambayo ni sawa na asilima 6.06 ya wote waliojiandikisha nchini huku Mbeya ikikamata nafasi ya tatu kwa kuwa na watu waliojiandikisha 1,373,000, sawa na asilimia 5.77 ya wapiga kura wote wa Oktoba.

Morogoro inakamata nafasi ya nne kwa kuandikisha watu 1,272,140, sawa na asilimia 5.35 ya wapiga kura wote; Tabora watu 1,083,926 (asilimia 4.56), Dodoma 1,053,136 (asilimia 4.43), Kagera 1,039,268 (asilimia 4.37), Tanga 1,009,276 (asilimia 4.24) na Arusha wameandikishwa watu 1,000,870, sawa na asilimia 4.21 ya watu wote walioandikishwa nchini.

Kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi, mshindi wa nafasi ya urais ni yule anayepata kura nyingi zitakazopigwa kulinganisha na washindani wake. Kwa sababu hiyo, mgombea yeyote atakayefanikiwa kupata asilimia 100 ya kura katika mikoa hiyo tisa atajihakikishia kuwa rais ajaye hata kama atafanya vibaya katika maeneo mengine ya nchi.

MIKOA MINGINE
Mbali na mikoa hiyo tisa, mikoa mingine ambayo Nipashe imefanikiwa kupata idadi ya waliojiandikisha ni Mara wenye watu 884,985, sawa na asilimia 3.72 ya watu wote waliojiandikisha, Shinyanga watu 768,270 (asilimia 3.23), Kigoma 794,463 (asilimia 3.34), Lindi 569,261 (asilimia 2.4), Ruvuma 826,779 (asilimia 3.48), Mtwara 682, 295 (asilimia 2.87), Iringa watu 526,006 (asilimia 2.21), Kilimanjaro 794,556 ( asilimia 3.34) na Manyara watu 673,357, sawa na asilimia 2.83 ya wote waliojiandikisha.

MAGUFULI, LOWASSA
Inaelezwa kuwa kutokana na ripoti hii ya watu waliojiandikisha kupitia BVR, kamwe haitashangaza kuona baadhi ya wagombea wakiwamo wa vyama vyenye wafuasi wengi vya CCM na Chadema wakielekeza zaidi nguvu zao katika mikoa hiyo tisa inayobeba turufu ya ushindi kwa kila mgombea.

Tangu kuanza rasmi kwa kampeni Agosti 22, 2015, timu za kina Dk. Magufuli na Lowassa zimeonyesha wazi kuwa zimewasilisha ratiba zao kimkakati zaidi, hasa kwa kuzingatia wingi wa wapiga kura katika maeneo wanayokwenda.

Hadi sasa, kwa pamoja, tayari wagombea hao na wagombea wao wenza wameshafanya mikutano ya kampeni kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Mbeya, Morogoro, Tabora, Arusha na Tanga. Kadhalika, kwa nyakati tofauti, wagombea hao wameshapita Mwanza na mikoa ya jirani wakati wakisaka wadhamini ndani ya vyama vyao na pia kwa 'gia' ya kutambulishwa baada ya kupitishwa na vyama vyao.

NEC WANENA
Akizungumzia uwezekano wa baadhi ya wagombea kuwekeza nguvu zao za kampeni katika baadhi ya mikoa yenye wapigakura wengi na kutwaa ushindi usiohusisha kura za kutosha kutoka maeneo mengine ya nchi, Mwanasheria wa NEC, Emmanuel Kawishe, alisema hawatarajii jambo hilo kwani ni vigumu kwa mgombea urais kuwa mshindi kwa kupata kura zote katika baadhi tu ya mikoa.

Akitolea mfano wa mkoa wa Arusha uliaondikisha wapiga kura 1,000,870 kwa mfumo wa BVR, Kawishe alisema mgombea yeyote atakayeelekeza nguvu zake mkoani humo peke yake bado hawezi kujihakikishia ushindi kwakuwa wapigakura wote nchini wapo zaidi ya milioni 23 na majimbo yapo 264.

“Kiuhalisia ni vigumu jambo hilo kutokea kwa sababu haiwezekani mgombea urais akapata kura nyingi katika mikoa michache tu na kwingine asipate kitu halafu akawa rais,” alisema Kawishe.

MATOKEO UCHAGUZI 2010
Katika uchaguzi mkuu uliopita 2010, waliojiandikisha kupiga kura walikuwa wananchi 20,137,303. Rais Jakaya Kikwete alitangazwa kuwa mshindi baada ya kupata kura 5,275,899 kati ya kura 8,626,283 zilizopigwa, sawa na asilimia 61.16. Waliomfuatia ni Dk. Willibrod Slaa wa Chadema aliyepata kura 2,271,885 (26.34%), Prof. Ibrahim Lipumba (CUF) kura 697,014 (8.08%), Peter Mziray Kuga wa APPT kura 96,932 (1.12%), Hashim Rungwe wa NCCR-Mageuzi kura 26,321 (0.3%), Mutamwega Mgahywa wa TLP kura 17,434 (0.20%) na Fahmi Dovutwa wa UPDP kura 13,123, sawa na asilimia 0.15
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment Blogger

 
Top