0

Dar es Salaam. Janeth Magufuli bado anasubiri miezi mitatu ya kampeni nzito za kumuwezesha mumewe kuingia kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano, lakini walimu na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mbuyuni tayari wanasikitika kumpoteza mwalimu huyo wa jiografia, historia na Tehama.
Mumewe, Dk John Pombe Magufuli amepitishwa zaidi ya wiki moja iliyopita kuwa mgombea urais wa Tanzania kwa tiketi ya CCM, na hivyo atalazimika kupambana vikali na wagombea wa vyama vingine ili kujihakikishia anaingia Ikulu kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano.
Lakini walimu na wanafunzi wa shule hiyo wanaona kuwa tayari Dk Magufuli ameshajihakikishia tiketi ya kuingia Ikulu na walichonacho sasa ni kusononeka kwa kuwa wanampoteza mmoja wa walimu bora shuleni hapo.
“Kama mumewe akichaguliwa, nitakosa utu na busara zake. Na unajua? Ni mwalimu wa mazingira na anajua majukumu yake. Darasa la tano watamkumbuka sana,” anasema mwalimu mkuu wa shule hiyo, Dorothy Malecela.
“Ni mwanamke mchapakazi sana na ni mwalimu mzuri, mtu mwenye upendo na mnyenyekevu. mtu pia mwenye moyo mzuri. Wakati fulani alitoa msaada wa baiskeli kwa mwanafunzi mlemavu shuleni hapa.”
Alikuwa akimzungumzia mwanafunzi mlemavu Elisha Lameck, ambaye alikuwa akipata shida kutoka sehemu moja kwenda nyingine wakati akiwa shuleni hapo.
Mwalimu Malecela anasema licha ya kuwa ni mke wa Waziri Magufuli, ilikuwa kazi kufahamu kama ni mke wa kigogo.
“Hakuwa na makuu hata kidogo, hata watoto wake walikuwa wakisoma hapa, na mwingine anasoma shule ya Kata ya Oysterbay,” anaeleza.
“Watoto wao wanasoma shule za kawaida sana. Shule ya kata tofauti na wengine ambao huwapeleka nje ya nchi.”
Malecela alieleza kuwa Mwalimu Magufuli hakuwa mtegeaji kazini.
“Hakuwahi kukosa kipindi na kama akiwa na dharura huwa anamwomba mwalimu mwingine amsaidie kipindi chake,” alisema.
Si mwalimu mkuu pekee ambaye alimmwagia sifa Mama Magufuli.
Ally Rajab na John Manda, ambao wako naye ofisi moja wanamuelezea Mwalimu Magufuli kuwa mtu ambaye ilikuwa vigumu kumtambua kuwa ni mke wa waziri, lakini pia mpole na anayeipenda kazi yake.
Mwalimu Rajab alisema kuwa wakati mwingine walikuwa wakinunua mihogo na kachori kwa ajili ya chai asubuhi, na Mwalimu Janeth alikuwa akijumuika kula pamoja nao.
“Hata wakati mwingine wa safari za mafunzo, huwa anatoa fedha kwa watoto ambao wazazi wao wameshindwa kuwalipia,” alisema.
“Hata wakati mwingine inapotokea walimu kukwaruzana ofisini, amekuwa msuluhishi.”
Baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo, Mabano Mzee, Mariam Mwalami wanafunzi wa darasa la sita, wanasema kuwa Mwalimu Magufuli alikuwa wa aina yake.
Mzee anasema mke huyo wa Dk Magufuli si mtu wa kuchapa viboko wanafunzi.
“Kama kuna tatizo, anakuelekeza, kama una shida anakusikiliza,” alisema Mzee.
Naye Mariam anasema kuwa anampenda Mwalimu Magufuli kwa kuwa anajua jinsi ya kumfundisha mtu na anaelewa, na huwa anajua kama watu wameelewa ama la.
“Baada ya kufundisha huwa anamwita mwanafunzi na kumuuliza kama ameelewa na kinachonifurahisha, hata tunapokula makande naye hula,” alisema Mariam.
Stella Ijumba, mwalimu na rafiki mkubwa wa Janeth Magufuli, anasema aliposikia Dk Magufuli amepita, alijua hatakuwa tena na mwalimu huyo.
“Niliposikia mzee kapita, nikamtumia meseji, ‘Hongera rafiki yangu, hayo yote yamepangwa na Mungu’, japokuwa hakujibu, lakini nilijua tu wengi watakuwa wamemtumia sasa anashindwa kujibu, alisema mwalimu huyo wa darasa la nne.
“Nitamkumbuka sana rafiki yangu, alikuwa mpole sana... ninawatakia kila la kheri yeye na mumewe.”
Mwingine aliyemzungumzia Mwalimu Magufuli ni muuza matunda shuleni hapo, alisema kuwa atamkosa mteja wake ambaye mara kwa mara hununua matunda kwa ajili ya kula ama kupeleka nyumbani.
“Huwa napeleka matunda hata nyumbani kwake huwa ananiagiza, lakini juzi juzi hapa nilipokwenda nikakuta hali tofauti, kulikuwa na ulinzi mkali, nikashindwa kumuuzia, nikaondoka,” alisema muuza matunda huyo.
“Baadaye nikasikia habari za mumewe kuwa ameteuliwa kuwania urais, nikaona sasa ni ngumu tena kumuona na itakuwa tunamuona kwenye Tv tu.”
Lameck, ambaye alinunuliwa baiskeli na Janeth alisema: “Ninampenda sana Mwalimu Magufuli kwani kanisaidia baiskeli hii...mama huwa ananichukua kunileta shule, lakini hii imenisaidia na itampunguzia mama kazi,” anasema.
Anasema kuwa kaka yake, Eliya sasa ndiye anayemsindikiza kutoka na kwenda shule na mama yao amebaki nyumbani akiendelea na shughuli nyingine.
Iwapo Dk Magufuli atachaguliwa kuliongoza Taifa Oktoba 25, Shule ya Mbuyuni itakuwa imeweka historia ya aina yake kwa kutoa wake wawili wa marais.
Salma Kikwete, mke wa Rais anayemaliza muda wake, pia alifundisha shule hiyo katika kipindi chake cha miaka 20 ya utumishi serikalini.
Lakini kingine kitu kingine cha aina yake ni kwamba iwapo Dk Magufuli atakuwa Rais, maana yake mkewe ataingia kwenye kundi la wake za marais wawili wa nchi zilizo kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao majina yao ni Janeth.
Mke wa Rais wa Uganda ni Janet Kataaha Museveni wakati mke wa Rais Paul Kagame wa Rwanda anaitwa Jeannette Kagame.

Post a Comment Blogger

 
Top