0
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jji Mstaafu, Damian Lubuva akizungumza na wanahabari juu ya mambo yahusuyo tume hiyo.ZAIDI ya waumini 4,000 wa Kanisa kongwe la Watch Tower lenye umri wa zaidi ya miaka 100, wamenyimwa haki yao ya msingi ya kikatiba ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.
Kwa mujibu wa imani na makatazo ya kanisa hilo, waumini wake hawaruhusiwi kupiga kura, kuwa wanasiasa, kusoma zaidi ya darasa la saba na pia hawatakiwi kuwa matajiri. Ni kutokana na makatazo yao, waumini wote wenye umri wa kupiga kura, hawakujiandikisha katika Dafatari la Kudumu la Wapigakura katika mfumo wa BVR kutokana na imani na makatazo ya kanisa hilo.
Kanisa hilo lililopo katika Kitongoji cha Kitika, tarafa ya Kasanga wilayani Kalambo, mkoani Rukwa lina hadhi ya kuwa makao makuu ya Kanisa la Watch Tower duniani. Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi umebaini kuwa licha ya kanisa hilo kuanzishwa miaka 100 iliyopita lakini bado halijasajiliwa rasmi kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kukinzana na imani na makatazo ya kanisa hilo yaliyoanishwa na mwasisi wa kanisa hilo.
Kitongoji cha Kitika, kijijini Kasanga ndipo yalipo makazi ya kudumu ya Baba Mtakatifu au “Papa” wa kanisa hilo maaarufu kama “Vatican City“ likiwa na waumini walionea hadi nchi jirani ya Zambia.
Kadhalika uchunguzi huo umebaini kuwa kanisa hilo lililoanzishwa na Baba Mtakatifu wa Kwanza, Enock Sindani akitoka Marekani alikokuwa anaishi na kufanya kazi, umebaini kuwa kwa sasa limegawanyika, na kusababisha kuwapo Baba Watakatifu watatu, kila mmoja akiwa na waumini wake, lakini wote wakibakiza makao makuu kijijini hapo.
Tangu kuanzishwa kwa kanisa hilo, karne moja iliyopita limeshakuwa na Baba Watakatifu watano ambao ni pamoja na mwasisi Sindani, Samwel Mwimanzi, John Chamboko, Edwin Simugala na Sikazwe; kwamba hadi sasa hakuna Baba Mtakatifu wa kanisa hilo anayetoka nje ya nchi hii.
Mmoja wa “Papa” wa kanisa hilo, Jonas Simulunga (67) akizungumza na mwandishi wa habari hizi hivi karibuni alikiri zaidi ya waumini 4,000 wa kanisa hilo wakiwemo viongozi wa kiroho hawakujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura hivyo wamepoteza sifa ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25, mwaka huu.
Alisisitiza siasa kwa waumini na viongozi wa kanisa hilo ni mwiko. Kwa mujibu wao waumini na viongozi wao wanazuiwa kujiunga na chama chochote cha siasa au kushika nyadhifa za kisiasa licha ya kuwa hawatashiriki katika kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu, wanakiri kuwa hawajawahi kupiga kura katika uchaguzi wowote ukiwamo Uchaguzi Mkuu tangu nchi hii ijipatie Uhuru miaka 53 iliyopita.
Hata hivyo, wote wamekiri kuwa waumini na viongozi wao hawakuweza kujitokeza kujiandikisha katika Sensa ya Watu na Makazi Agosti 26, 2012 kwa kuwa wao wanachodai walitaka wahesabiwe tu bila kuulizwa maswali tena yasiwe ya siri kwa kuwa hawako mahakamani.
“Waumini wetu pia si wanachama wa chama chochote cha siasa… kwa sababu ni makatazo ya kanisa hili kwamba hawawezi kutumikia mabwana wawili … hawaruhusiwi kupiga kura katika uchaguzi wowote ule kuanzia wa Serikali za Mitaa hadi Uchaguzi Mkuu wa kuwachagua madiwani, wabunge na Rais…
“Tunawaona wanasiasa kama watu walaghai, waongo na uongo ni dhambi kwetu pia uchaguzi umekuwa ukigubikiwa na visa vya rushwa kwetu sisi kama viongozi na waumini wa kanisa hili ni dhambi kutoa au kupokea rushwa,“ alisisitiza kiongozi huyo mkuu wa kanisa hilo, Simulunga.
Akifafanua hata waumini wa kanisa hilo walipo nchini Zambia nao ni mwiko kujihusisha na siasa kwamba hawajawahi kushiriki katika kuchagua viongozi wao wa kisiasa kwa kuwapigia kura.
Makatazo mengine kwa mujibu wa Kiongozi huyo wa juu kabisa wa kiroho wa kanisa hilo ni pamoja na waumini kutoruhusiwa kuchangia damu kwa watu wenye mahitaji kwa kuwa ni dhambi kutoa sehemu ya uhai na kumpatia mtu mwingine huko ni kuingilia mamlaka ya Mwenyezi Mungu.
Baadhi ya waumini wa kanisa hilo wanakiri kuwa hawaruhusiwi kusajili laini za simu zao za mikononi wao wenyewe hivyo wanalazimika kuwa kuwatumia watu wengine ambao si waumini wa kanisa hilo kusajili kwa nia yao kwamba hawako tayari kuulizwa maswali kama vile wao mahakamani kwambani mwiko kwa imani ya kanisa hilo.
Tangu kuanzishwa kwa Kanisa hilo, limeshakuwa na Baba Watakatifu watano maboa ni pamoja na muasisi Sindani, Samwel Mwimanzi, John Chamboko, Edwin Simugala na Sikazwe; kwamba hadi sasa hakuna Baba Mtakatifu wa Kanisa hilo anayetoka nje ya nchi hii.
Kwa mujibu wa Baba Watakatifu hao, kanisa hilo ambalo lina misimamo mikali linaongozwa na Amri 10 za Mungu ambapo waumini na viongozi wake wanalazimika kuzishika kwa uaminifu na uadilifu mkubwa, kinyume cha hivyo wanatengwa au kuvuliwa madaraka.
Walidai kuwa hata hivyo wanajihusisha na kujitolea katika shughuli za maendeleo zikiwamo kujenga shule, zahanati na pia wanaruhusu watoto wao kwenda shule na hata wao wenyewe wanatibiwa hospitalini, lakini ni marufuku ni kumsaidia mtu damu au kuongezwa damu kwa madai kuwa ni mali ya mtu.
Kwa upande wake, Mratibu wa uchaguzi Mkuu mkoa wa Rukwa, Erasmus Rugarabamu alikiri kuwa kanisa hilo limekosea kwa kukiuka taratibu zilizowekwa na Tume ya Uchaguzi wa Taifa (NEC) .
Rugarabamu ambaye pia ni Msaidizi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Rukwa (Rasilimali Watu) aliongeza kuwa mujibu wa NEC kila Mtanzania mwenye sifa za kupiga kura ana haki ya kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura na kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu wa kuwachagua madiwani, wabunge na rais.
“Sisi tunafuata maaelekezp yaliyoainishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwamba mtanzania yeye mwenye sifa za kupiga kura ana haki hiyo bila kujali imani yake ya kisiasa kidini, kabila wala rangi sasa viongozi wa kanisa hilo wamekiuka maelekezo ya NEC kwa kweli hili tungelijua mapema … hatua za haraka zingechukuliwa,“ alisisitiza.

Post a Comment Blogger

 
Top