0
PENZI ni kikohozi, kulificha huwezi! Habari ya mjini kwa sasa ni mahaba niue ya muuza nyago kwenye nyimbo za wanamuziki wa Bongo Fleva, Agness Gerald ‘Masogange’ na staa wa muziki nchini Nigeria ‘Naija’, David Adedeji Adeleke ‘Davido’ baada ya kuoneshana penzi zito hadharani, Risasi Jumamosi lina mkanda mzima.“Yaani Masogange na Davido ni mahaba niue, wanaponda raha kwa kwenda mbele maana hata juzi tu walikuwa kwenye klabu moja hivi wanakunywa na kula pamoja huku wakifurahia vilivyo uumbaji wa Mungu.
“Davido ametinga hapa Sauz akitokea Nigeria kwa ajili tu ya kuja kukutana na Masogange ambaye mara nyingi anakuwa Sauz,” kilisema chanzo hicho.
Chanzo hicho kilienda mbele zaidi na kutuma video ambayo inamuonesha Davido akimnywesha pombe Masogange huku wakiwa wamelewa tilalila bila kujali kwamba walikuwa klabu ambako kuna watu wengi.
“Angalieni hiyo video kwa ushahidi zaidi, Davido alikuwa akimnywesha pombe kali Masogange na kuna wakati Masogange naye alikuwa akimnywesha Davido.
“Nilikuwa nao klabu wakifanyiana vitendo vya kimahaba kama kunyweshana pombe kwenye chupa moja bila kujali macho ya watu,” kilidadavua chanzo hicho na kuongeza:
“Nakwambia huku (Sauz) Masogange na Davido wanakula bata hadi kuku wanaona wivu. Yaani ni mapenzi mazito usiwapimie.”
DIAMOND ATAJWA
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Davido ambaye ni rafiki wa karibu na mwanamuziki wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ inadaiwa ndiye aliyemuunganishia jamaa huyo kwa Masogange kwani alikuwa akimsikia na kumuona kwa muda mrefu kwenye mitandao ya kijamii na akampenda.
“Si bure, kilichomvutia Davido ni ule mzigo wa Masogange (makalio) maana kila siku huwa anautundika kwenye Instagram ‘so’ akaona mtu wa kumpigia pande ni Diamond,” kilidai chanzo hicho.
MASOGANGE ATAFUTWA
Baada ya kuzipata habari hizo na ushahidi wa video, gazeti hili lilimtafuta Masogange ambapo jitihada hizo ziligonga mwamba kutokana na mwanadada huyo kutumiwa ujumbe kwenye mtandao wa kijamii wa WhatsApp bila kujibu.
HUKO NYUMA
Masogange ambaye alipewa jina hilo baada ya kuuza sura kwenye Wimbo wa Masogange wa msanii Abednego Damian ‘Bele 9’, aliwahi kutajwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanaume raia wa Nigeria mwenye maskani Sauz ambaye alimsababisha hadi kuomba uraia nchini humo lakini waliachana baada ya muda mfupi.

Post a Comment Blogger

 
Top