0

DU! Kazi kwelikweli! Habari ya mjini kwa sasa ni mtoto mzuri Bongo Movies, Wema Isaac Sepetu ‘Madam’ kuwania Ubunge wa Viti Maalum Mkoa wa Singida kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), lakini nyuma yake kuna habari zinazodai kuwa mrembo huyo ameingiwa na hofu ya kukatwa jina kama ilivyotokea kwa Mbunge wa Monduli, Edward Ngoyai Lowassa aliyekuwa mmoja wa watia nia ya kugombea urais, Amani lina mkanda kamili.
ALIVYOENGULIWA LOWASSA
Lowassa alikuwa miongoni mwa makada 33 kati ya 38 walioenguliwa na Kamati ya Maadili ambayo ilipitisha majina matano pekee katika kikao cha Kamati Kuu, Halmashauri Kuu na baadaye Mkutano Mkuu kupitisha Mbunge wa Chato, Dk. John Pombe Magufuli kuwa mgombea urais kwa Tiketi ya CCM.
TUJIUNGE NA CHANZO
Chanzo kilicho karibu na staa huyo kimepenyeza ‘ubuyu’ kuwa, Wema ambaye anashikilia Taji la Miss Tanzania 2006/07, ameingiwa na hofu hiyo baada ya kuona Lowassa ambaye ana sifa ya kukubalika kama alivyo yeye ameenguliwa na kikao cha Kamati ya Maadili ya CCM.
“Bibie (Wema) anajiamini, anakubalika kweli lakini kitendo cha Lowassa ambaye alikuwa anaonekana kukubalika kimemtia hofu na kuona kumbe kukubalika pekee si silaha ya ‘kuwini’ kupitishwa na chama,” kilisema chanzo hicho.
CHANZO CHAZIDI KUTIRIRIKA
Chanzo hicho kilizidi kwenda mbali zaidi kwa kudai hofu hiyo iliongezeka kwa Madam hususan baada ya kusambaa kwa kuwepo kwa watu wasiompenda kupandikiza chuki kwamba baadhi ya skendo zilizomgusa zinaweza kumpotezea sifa ya jina lake kupitishwa na Halmashauri Kuu ya chama chake.
“Si unajua tena Madam kwenye maisha yake ya sanaa amepitia skendo za hapa na pale, hiyo inaweza kuchangia kumtia hofu maana wabaya wake wanaweza kuitumia kama silaha hivyo amekuwa akitoa chozi na kumuomba Mungu amfanikishe,” kilisema chanzo hicho.
SKENDO INACHANGIA KUMPOTEZEA SIFA?
Duru mbalimbali za habari zinaonesha kwamba kitu kikubwa kinachoangaliwa kwa kiongozi ni suala la uwajibikiaji na si tabia binafsi au skendo.
Wapo viongozi ambao walikuwa na skendo lakini wameweza kupitishwa na wananchi wao na kuwatumikia vizuri kuliko hata wale walionekana wasafi.
“Si kweli kwamba skendo ndiyo kigezo kikuu cha kumpitisha mgombea, mbona watu kama akina Mike Sonko (alikuwa Mbunge wa Kenya), marehemu Amina Chifupa (alikuwa Mbunge Viti Maalum, Vladimir Vladimirovic Putin (rais wa urusi) na wengine wengi, walikuwa au walipata skendo lakini walifanya vizuri katika uongozi wao,” alisema mwanaharakati mkubwa wa siasa nchini aliyeomba hifadhi ya jina.
NAPE ANENA
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipoulizwa kama kuna uwezekano wa kumuengua mgombea yeyote kutokana na skendo au chuki zinazoezwa na baadhi ya wanachama wa chama hicho, alisema si kweli bali wao wanafUata taratibu na kanuni walizojiwekea na si vinginevyo.
“Sisi tuna kanuni na taratibu za chama, hiyo ndiyo misingi yetu. Hatumuengui mtu kwa chuki binafsi wala kitu kingine chochote zaidi ya kufuata kanuni zetu,” alisema Nape.
WEMA ANASEMAJE?
Akizungumza na mwanahabari wetu hivi karibuni, Wema alikiri kupata hofu hiyo kwa muda lakini ameshajiamini kutokana na kumuomba Mungu ambaye amekuwa akimtanguliza katika kila jambo analolifanya.
“Kusema kweli mtu unapotaka kufanya jambo unapaswa kujiamini, hata mimi mwanzo nilikuwa nimejipa matumaini ya hali ya juu kwamba Lowassa atapita, lakini bahati mbaya akakatwa, naamini Mungu yupo, mimi naswali usiku na mchana, Mungu atanisimamia katika hili,” alisema Wema.

Post a Comment Blogger

 
Top