0
WASOMI na wanaharakati mbalimbali nchini kwa kumteua Dk John Magufuli kuwa mgombea Urais kwa tiketi ya CCM, chama hicho kimempata mgombea sahihi, asiye na makundi pia kimezingatia jinsia baada ya kumchagua mgombea mwenza mwanamke, Samia Suluhu Hassan.
Kutokana na hali hiyo, wametabiri kuwa, CCM kitapata ushindi wa kishindo na kuwaacha mbali wapinzani wao.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili ikiwa ni simu moja baada ya vikao vya uteuzi vya CCM kumaliza kasi ya kuchuja wagombea 38 na hatimaye kuthibitishwa na Mkutano Mkuu, walisema Magufuli `ni jembe’.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Faraja Kristomus alisema mwaka huu wa uchaguzi CCM imepata mtu sahihi hivyo itajizolea kura nyingi kutoka hata kwa wananchi ambao sio wa chama hicho kwa kuwa mgombea huyo ana sifa zinazojitosheleza ikiwemo uchapakazi.
“Mchakato huu umeepusha hatari ya kuwepo kwa makundi kama ilivyozoeleka kwa CCM. Hivi sasa hakuna makundi mgombea huyu ana nafasi nzuri ya kukiokoa chama hiki ikiwa atafanikiwa,” alisema.
Alisisitiza katika uwaziri wake Magufuli alionesha anapambana na ufisadi, hivyo endapo atapata ushirikiano ni mtu sahihi.
Mhadhiri Mwandamizi mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Azaveli Lwaitama alisema CCM imefanya uamuzi wa busara kwa kuwa imesimama kidete na kufuata taratibu zake bila shinikizo.
Alisema pia kitendo cha kumteua mgombea mwenza mwanamke inahitaji pongezi japo walitakiwa katika tatu bora ndipo atoke mgombea mwenza huyo.
Mratibu wa Kituo cha Usuluhishi kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), Gladness Munuo alisema CCM imedhihirisha kuwa imeweza kufuata maoni ya Katiba Inayopendekezwa kuwa mwenyekiti akiwa mwanamume, basi makamu wake awe mwanamke, au akiwa mwanamke makamu wake awe mwanamume. Aidha, alisema kila mmoja anafahamu kuwa Dk Magufuli akiwa kazini ni mfuatiliaji mzuri.
“Endapo Magufuli atachaguliwa atakuwa msimamizi mzuri kwa kuwanufaisha wananchi sio kujinufaisha mwenyewe,” alisema.
Pia, alisema binafsi anaunga mkono uchaguzi wa mgombea mwenza kwa kuwa anamfahamu ni mwanamke aliyeweza kusimamia vizuri kila majukumu aliyopangiwa.
“Kitu kikubwa ni kuwatia moyo ili waweze kufanya kazi zao vizuri. Ni viongozi wa watu wachapakazi,” alisema Munuo

Post a Comment Blogger

 
Top