0
Aliyekuwa mmoja wa wapambe wakubwa wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa wakati wa safari ya matumaini, Mgana Msindai, sasa ameelekeza nguvu kuwania ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) jimbo jipya la Mkalama mkoani Singida.

Msindai alikuwa mpambanaji mkubwa kuhakikisha Lowassa anafanikisha ndoto ya kuteuliwa na CCM kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao, hata kufikia hatua ya kumshitaki mahakamani Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda, kwa madai ya kumdhalilisha.

Akizungumza na mtandao huu kwa njia ya simu jana, Mwenyekiti huyo wa Wenyeviti wa CCM Tanzania, alisema wakati ule alimpigania Lowassa kwa nguvu zote, lakini sasa ameamua kubeba msalaba wake mwenyewe.

“Mimi naomba nizungumzia ya kwangu. Kweli tulikuwa katika msafara mmoja na Lowassa tukimuunga mkono kwenye safari ya matumaini ndani ya CCM.

“Sasa tulipofika mwisho na jina lake halikurudi, wengine tumeamua kuendelea kuwamo ndani ya CCM na sasa ninawania kuteuliwa kugombea ubunge wa Mkalama,” alisema.

Akizungumzia baadhi ya wenzake kwenye kambi ya Lowassa (Dk. Emmanuel Nchimbi, Sophia Simba na Adam Kimbisa) kupinga uamuzi wa Kamati Kuu ya CCM kutolipitisha jina la Lowassa, Msindai alisema: “Tulikuwa tunajua kwamba Lowassa angeshinda mapema sana. Lakini jina halikuletwa (NEC).

“Baada ya hapo, kwa umoja wetu tukaamua kumsaidia Magufuli (Dk. John Magufuli) na akashinda.”

Post a Comment Blogger

 
Top