0

 

Mama ambaye amejifungua mara ya kwanza anaweza kuhitaji msaada katika kunyonyesha. Msaidie ili aweze kuwa mtulivu na makini kwa kazi hiyo. Msaidie kwa kutumia mablanketi na miito ili aweze kukaa wima na kujisikia vizuri. Waombe wanafamilia na wageni kumpa mama na mtoto faragha. Mtie moyo. Unyonyeshaji huwa rahisi kadri mama atakavyoendelea kunyonyesha na kupata uzoefu.

Maziwa ya mama ni bora kwa mtoto kuliko aina yoyote nyingine ya maziwa au mchanganyiko wowote wa vyakula vingine
Mwepushe mama maumivu kutokana na michubuko ya chuchu kwa kumweka katika mkao mzuri wa unyonyeshaji. Geuza mwili wote wa mtoto umwangalie mama ili shingo yake isipinde. Subiri hadi atapopanua mdomo wake. Halafu mweke kwenye ziwa. Chuchu na eneo jeusi linalozunguka linapaswa kufunikwa ndani ya mdomo wa mtoto.


Chuchu ndani ya mdomo wa mtoto
Mdomo wa chini ukiwa umefunika sehemu ya chini ya eneo jeusi la ziwa
Mdomo ukiwa wazi kabisa
Mtoto akiwa ameshikiliwa karibu na mwili wa mama yake
Kama hivi.
Siyo kama hivi. Mkao mbaya unaweza kumsababisha maumivu kutokana na michubuko kwenye chuchu.

Maziwa ya mwanzo ya mama ni sawa na kimiminika cha dhahabu

Maziwa ya mwanzo hutoka katika kiwango kidogo, lakini kiwango hicho ni sahihi kwa mtoto ambaye ndiyo amezaliwa. (Tumbo la mtoto ambaye ndiyo amezaliwa hubeba kiasi cha vijiko vya chai vichache tu vya maziwa kwa wakati.) Maziwa ya kwanza yananata na huonekana ya njano njano. Lakini ingawa huonekana tofauti, ndiyo chakula sahihi kwa mtoto ambaye amezaliwa . Maziwa hayo yana virutubishi muhimu vilivyotengenezwa na mwili wa mama yake kwa ajili ya kumkinga mtoto dhidi ya maambukizi . Usimwage au kupoteza maziwa ya kwanza: ni muhimu kwa mtoto kuliko dawa yoyote ile. Unyonyeshaji ndani ya siku 2 za mwanzo ni muhimu kwa sababu husaidia kufungulia maziwa yaliyokamaa ambayo mama huanza kuzalisha ndani ya siku 3 baada ya kujifungua. Kadri mtoto anavyonyonya ndivyo na wingi wa maziwa ambayo mama yake atazalisha.

Je mtoto anapata maziwa ya kutosha?

Usiruhusu mtu yoyote akwambie kuwa huwezi kuzalisha maziwa ya kumtosha mtoto wako, hasa katika siku chache za mwanzo wakati mwili wako ndiyo unaanza kuzalisha maziwa.
Kwa sababu ya shinikizo kutoka kwa watu wengine na kutojiamini, akina mama( au mabibi, mashangazi au wakunga ambao wanasaidia kutoa msaada) huanza kuwalisha watoto ambao ndiyo wamezaliwa au watoto wachanga maziwa ya kopo, au uji, au vyakula vingine. Vyakula hivi vya ziada ni kupoteza fedha bure na pia vinaweza kusababisha mtoto kuharisha. Kuharisha husababisha mtoto kupoteza uzito na kuwa dhaifu.Na matumizi ya vyakula hivi husababisha mama atengeneze maziwa kidogo.Hivyo, hujikuta akiamini zaidi kwamba hawezi kumlisha mtoto wake vya kutosha kwa kutumia maziwa yake pekee. Kama wewe ni mfanyakazi wa afya, unaweza kuzuia mduara huu wa matatizo makubwa ya afya kwa kuwaonyesha akinamama kuwa una imani na uwezo wao wa kuwanyonyesha watoto wao. Msaidie mama kumweka mtoto katika mkao mzuri wa kunyonya, lakini pia mpatie mama nafasi ya kujifunza yeye mwenyewe jinsi gani unyonyeshaji unamsaidia mtoto. Ongea naye vizuri, taratibu. Kuwa na subira.

Kutengeneza maziwa ya kutosha

  • Nyonyesha mara kwa mara. Kadri unavyonyonyesha, ndivyo utatengeneza maziwa zaidi.
  • Tumia vinywaji vya kutosha na kula zaidi. Mlishe mtoto wako kwa kujilisha mwenyewe.
  • Pumzika mara kwa mara.Iwapo baba na wanafamilia wengine watasaidia na kazi zingine za nyumbani, mama atamhudumia mtoto vizuri zaidi.
Kadri unavyonyonyesha mara nyingi ndivyo utakuwa na maziwa mengi zaidi.
Watoto wengi hupoteza uzito kidogo katika wiki yao ya kwanza. Hili ni jambo la kawaida. Lakini baada ya hapo, upunguaji uzito humaanisha mtoto hapati lishe yakutosha. Vilevile, watoto hawakojoi sana siku yao ya kwanza, lakini baada ya hapo wanapaswa kutoa mkojo kila baada ya saa chache. Iwapo mtoto hatakojoa sana baada ya siku 2, atakuwa hapati maziwa ya kutosha. Je, kama mtoto atakuwa ananyonya mara kwa mara lakini hakojoi au kuongezeka? Katika hali kama hiyo ambayo siyo ya kawaida, unaweza kuhitajika kutafuta maziwa mbadala. Usimpe sukari au maji ya mchele. Usimpe maziwa mbadala ya makopo isipokuwa kama utakuwa na uhakika wa kumpatia kiasi kilichopendekezwa (kuongeza maji husababisha mtoto kuharisha na kuugua). Na usitumie chupa: hazisafishiki kwa urahisi na hivyo hueneza vijidudu ambavyo husababisha mtoto kuharisha.
Maziwa mbadala yanaweza kutolewa iwapo mama atafariki au atatengana na mtoto wake, au kwa nadra sana iwapo atakuwa kweli hatengenezi maziwa ya kutosha. Unaweza kumuomba mama mwingine kumnyonyesha mtoto huyu. Lakini kwanza apate kipimo cha virusi vya UKIMWI kujua iwapo yu salama. Hii ni kwa sababu virusi vya UKIMWI vinaweza kuenezwa kwa mtoto kupitia unyonyeshaji. Njia nyingine ni kutumia maziwa ya wanyama, mfano maziwa ya ngo’mbe au mbuzi yakiandaliwa kama ifuatavyo:
Changanya:
Kipimo 2 vya maziwa ya ngo’mbe au mbuzi
Kipimo 1 cha maji
Kijiko 1 kikubwa cha sukari
AU
Kipimo 1 cha maziwa ya kondoo
Kipimo 1 cha maji
Kipimo 1 cha kijiko kikubwa cha sukari

AU
Vipimo 2 vya maziwa ya kopo yaliyotelewa mafuta na ambayo hayajakolezwa sukari kiwandani
Vipimo 3 vya maji
Kipimo 1 kijiko kilichojaa sukari

Chemsha maziwa uliyotengeneza ili kuua vijidudu. Halafu ruhusu yapoe ndiyo umpatie mtoto kwa kutumia kikombe au kijiko kisafi.
Kukamua ziwa kwa mkono
Kama unalazimika kwenda kazini au kumuacha mtoto nyuma kwa sababu yoyote ile, unaweza kujaribu kukamua maziwa yako ili utakapokuwa umeondoka mtu mwingine aweze kumpa mtoto maziwa hayo.

  1. Nawa mikono yako vizuri na kusafisha chombo cka kukamulia.
  2. Kamata ziwa kwa vidole vyako na dole gumba likiwa pembeni mwa eneo jeusi linalozunguka chuchu. Kandamizia ziwa kwenye kifua chako. Halafu bonyeza vidole vyako pamoja ukiwa unalekea kwenye chuchu. Jisikie huru na fikiria kuhusu mtoto wako wakati unakamua maziwa hayo-hii itasaidia maziwa kutoka kwa urahisi

    Maziwa ya mama yatabaki salama kwa saa 8 kama hakutakuwa na hali ya joto kali nje.

Maambukizi ya kuvu mdomoni

Tumia kitambaa kidogo kisafi kusambaza dawa ndani ya mdomo wa mtoto.
Mabaka meupe ulimini au ndani ya shavu na kero wakati wa kunyoya vinaweza kuwa dalili ya maambukizi ya kuvu mdomoni. Maambukizi hayo yanaweza kwenea hadi kwenye chuchu ya mama na kusababisha wekundu, mwasho, na maumivu.
Jaribu kusuza chuchu na siki (vinegar), na baadaye kwa maji ya kawaida. Au kama huna siki, jitahidi tu kusafisha na kukausha chuchu yako kila baada ya kunyonyesha. Iwapo hii haitasaidia, paka dawa ya Jiivi kidogo kwenye chuchu mara 2 kwa siku 3. Pia paka Jiivi ndani ya mdomo wa mtoto mara moja kwa siku. (Kila kitu kitageuka kuwa na rangi ya zambarau lakini ni salama). Kama Jiivi haitasaidia, mpe mtoto dawa ya nistatini (nystatin).
Kama maambukizi ya kuvu yatakuwa yanapotea na kurudi, mtoto anaweza kuwa na tatizo lingine ambalo linadhoofisha kinga yake ya kupambana na maambukizi. Kwa mfano, watoto wachanga wenye VVU wanaweza kupatwa na kuvu mdomoni mara nyingi zaidi. Angalia VVU na UKIMWI (kinaandaliwa).

Maumivu ya ziwa, uvimbe, kuziba, au maambukizi

Wakati mwingine maziwa yanaweza kuziba mrija (njia ndogo ndani ya ziwa ambazo husafirisha maziwa). Ziwa huanza kuvimba, hugeuka kuwa jekundu na kutoa maumivu. Mara baada ya hapo, maambukizi yanaweza kuanza.
Dalili
  • Eneo lenye moto, wekundu na gumu kwenye ziwa
  • Maumivu katika ziwa wakati wa kunyonyesha
Kama kuna homa, basi mrija ulioziba umepata maambukizi.
Matibabu
  • Pumzika. Tumia vinywaji kwa wingi.
  • Nyonyesha angalau kila baada ya saa 2. Unyonyeshaji hata kama ziwa lina maambukizi ni salama kwa mtoto na ndiyo njia pekee ya kuyaondoa maambukizi.
Gandamiza kwa kwenda chini
ili kukanda eneo lililoziba
  • Hakikisha upo katika mkao mzuri wa kunyonyesha. Mwili mzima wa mtoto lazima umwangalie mama yake. Mdomo wa mtoto unapaswa kufunguka sana, na chuchu ingizwe ndani ya mdomo wake.
  • Nyonyesha upande unaouma kwanza, na uruhusu mtoto kumaliza maziwa yote kwenye ziwa.
  • Kukanda polepole kwa kutumia kitambaa kisafi na maji ya vuguvugu, au kuoga maji ya moto vinaweza kusaidia.
Wezesha ziwa lipate joto dakika 15 au 20 ,angalau mara 4 kwa siku. Au, weka nguo baridi au majani ya kabiji kwenye ziwa ili kupunguza uvimbe.
Kama kuna homa, mpatie dawa ya erithromaisini (erythromycin), miligramu 250 mara 4 kwa siku.

VVU na unyonyeshaji

Hivi sasa kuna dawa ambazo husaidia wanawake wajawazito wenye VVU kuwa wenye afya zaidi na kuzuia mambukizi ya virusi hivyo kwa watoto wao.Ili kuwalinda wanawake na watoto, kila mwanamke mjamzito anapaswa kupata kipimo cha VVU. Na iwapo atakuwa na VVU, anapaswa kupewa dawa za VVU, kwa muda wote atakapokuwa ananyonyesha, na baadaye kama atazihitaji. Angalia VVU na UKIMWI (kinaadaliwa).
Je, ni salama kunyonyesha iwapo una VVU?
Dawa za VVU huzuia uenezaji wa maambukizi wakati wa unyonyeshaji. Aidha mama au mtoto lazima atumie dawa hizo kila siku hadi mtoto atakapofikia hatua ya kuachishwa ziwa. Afya ya mtoto hulindwa pia kwa kumpatia maziwa ya mama kwa miezi 6 ya kwanza (au hadi atakapoota meno yake ya kwanza). Uji na vinywaji vingine siyo vizuri kwa afya ya mtoto.
Dawa za VVU kwa mama na mtoto zitawasaidia wote wawili kuwa na afya.
Bila dawa za VVU, kuna hatari ya maambukizi kupitia unyonyeshaji. Lakini hatari kutokana na kumlisha mtoto vyakula mbadala ni kubwa zaidi. Akina mama wengi wenye VVU hawana maji safi na salama, nishati ya kupikia, au fedha za kununua,kutayarisha na kumlisha mtoto kwa usalama vyakula hivyo mbadala. Watoto wao wana uwezekano mkubwa wakupatwa na utapiamlo, na ugonjwa wa kuhara, na wanaweza kupoteza maisha. Hii inamaanisha kuwa maziwa ya mama ndiyo salama zaidi – hata kama mama au mtoto atakuwa hatumii dawa za VVU.

Kwa watoto na akina mama sehemu zote, ziwa ndiyo bora zaidi

Unyonyeshaji

  • Gharama yake ni nafuu. Hakuna haja ya kununua vyakula mbadala, chupa, au chochote kingine.
  • Husaidia kusimamisha utokaji damu baada ya mama kujifungua.
  • Husaidia kuzuia mimba miezi inayofuatia kujifugua.
  • Huwalinda akina mama dhidi ya saratani na matatizo ya mifupa baadaye katika maisha yao.
  • Maziwa ya mama yanakuwa ndiyo yametengenezwa, yakiwa na vuguvugu, na tayari kutumika.
  • Yana virutubishi vyote ambavyo mtoto anahitaji.
  • Husaidia kuwakinga watoto dhidi ya kuhara, kichomi (nimonia) na magonjwa mengine.
  • Ni kinga inayodumu muda mrefu dhidi ya ugonjwa wa kisukari, mzio na saratani mbalimbali katika maisha ya mtoto ya baadaye.
  • Humweka mtoto salama na mwenye joto la kutosha akiwa pembeni mwa mama yake.
  • Humfanya mama na mtoto wake kuwa karibu zaidi.

Post a Comment Blogger

 
Top